Katika
safari ya maisha, ni jambo la kawaida kabisa kukutana na vikwazo vinavyoweza
kukatisha tamaa. Ukubwa wa vikwazo au changamoto hizo, zinaweza kukusababishia
ukaiona dunia kama imegeuka, au wakati mwingine ukatamani ipasuke uingie ndani
yake.
Yapo mambo
mengi yanayoweza kukufanya ufikirie hivyo. Huenda yakawa ni makosa ya
kibinadamu, matatizo, changamoto, kukatishwa tamaa na baadhi ya watu au
kujiponza mwenyewe kutokana na hili au lile. Lakini ukikaa chini, ukatafakari
utatambua kuwa hakuna binadamu asiyeteleza kwa kufanya makosa au kupitia
changamoto kwenye safari ya maisha.
Hivyo wakati
mwingine unapaswa kuelewa kuwa kwa kila linalokupata, bado unayo nafasi ya
kufungua ukurasa mpya. Kupatwa na mitihani katika maisha, mara nyingi ni darasa
mojawapo tunalotakiwa kuliangalia kwa umakini ili kupata somo au fundisho
lililo ndani yake.
Ikiwa
mtihani huo umekuja kutokana na kosa ulilofanya, ni vyema kukubali kama
umekosea na kisha kujipa nafasi ya kusonga mbele. Tunaelewa kuwa maisha ya kila
mmoja wetu kwa namna moja au nyingine yanaendeshwa na misimamo mbalimbali. Kuna
wale wanaoamini kuwa wao hawawezi kufanya
jambo Fulani na wakati mwingine kuamini kuwa hawawezi kukosea kabisa.