Monday, April 28, 2014

NJIA YA KUWEKA AKIBA NA KUONGEZA MTAJI KATIKA BIASHARA YAKO



Moja ya nguzo za mafanikio ya wajasiriamali ni elimu, ikwemo ya kuwaongezea upeo wa kutafuta mitaji.
Ni ijumaa nyingine tunapokutana tena katika kona hii ya mjasiriamali, hii ni kona ambayo maudhui yake ni kuona namna bora ambazo wajasiriamali wanaweza kuzitumia ili kuanzisha na baadae kuendeleza biashara zao na kupata mafanikio wanayotamani.

Makala iliyopita ilijadili juu ya umuhimu wa kuweka akiba ili kujikinga na majanga.

Kuna msemo unasema akiba haiozi, mjasirimali unapaswa wakati wote kukumbuka msemo huu ili uwe chachu ya wewe kujiwekea akiba kwa malengo mbalimbali.

Ukiwa na utamaduni wa kujiwekea akiba kutokana na mapato yako unayoyapata utakuwa katika nafasi nzuri ya kuweza kukabilina na majanga mbalimbali ambayo yanaweza kutokea katika biashara yako, kumbuka una nafasi ya kubadilika na kujipanga upya.

Leo katika kona ya mjasiriamali tutakumbushana juu ya baadhi ya njia ambazo wajasiriamali wanaweza kuzitumia ili kuweza kuongeza mitaji ya biashara zao. Katika njia mbalimbali za kuongeza mitaji zipo zinazoweza kusaidia na nyingine kuumiza.

Mitaji ya biashara ni kilio cha wengi aidha kwa wale walio katika ujasiriamali au kwa wale wenye nia ya kuingia kwenye ujasiriamali. Wengi hulia kwamba watapata wapi mtaji kwaajili ya kuanzisha biashara au kwaajili ya kuendeleza biashara.

Wajasiriamali wanapaswa waelewe kwamba kuna njia mbalimbali za kuweza kuongeza mtaji katika biashara wanazofanya. Muhimu zaidi ni kufahamu njia hizi ili kuweza kuangali ni ipi kwa hatua uliyofikia inaweza kukusaidia zaidi badala ya kukuumiza.

Yafaa pia kujiuliza je ni sababu zipi zinazopelekea wewe kuwa na hitaji la ongezeko la mtaji katika biashara yako  na nini matokeo tarajiwa. Kujiuliza maswali haya na mengine itakusaidi kufanya uamuzi sahii. Zifuatazo ni njia za kuongeza mitaji ya biashara yako.

Njia ya kwanza ni uwekaji wa akiba. Uwekaji wa akiba ni njia ya kwanza ambayo inaweza kukusaidia katika kukuza mtaji wako wa biashara. Kma utakuwa na utamaduni wa kujiwekea akiba ni rahisi kwako kutumia akiba ili uweze kukuza mtaji wako.

Iwe kwa mjasiriamali mwenye biashara mpya au inayoendelea ni muhimu sana kufikiria kutumia njia hii ili kuweza kukuza mtaji wa biashara. Uwekaji wa akiba ni moja ya njia ya kukuza  mtaji ambayo haina gharama wala matatizo kuliko nyingine yoyote.

Uwekaji wa akiba ni njia inayoonekana ngumu kati ya watu kwasababu ni njia ambayo inahitaji nidhamu ya hali ya juu. Unapotaka kutumia njia hii ili kuweza kukuza mtaji wa biashara au kuendeleza biashara unahitaji nidhamu katika matumizi ya fedha zako.

Jiulize je matumizi ya fedha zako yakoje? Ni yapi yamekuwa matumizi ya msingi na yapi si ya msingi, kwanini usipunguze au kuacha matumizi yasio ya msingi na kuweka akiba ili kuweza kukuza mtaji kwaajili ya biashara yako.

Jiulize unatumia kiasi gani cha fedha zako kwaajili ya ‘vocha’, unatumia kiasi gani kwaajili ya pombe, unatumia kiasi gani kwaajili ya starehe, vipi michango ya harusi, je unatumia kiasi gani kwaajili ya burudani nyingine ambazo si za msingi!

Kaa chini na utafakari juu ya mapato na matumizi yako na angalia ni kwa namna gani unaweza kuweka sehemu ya mapato yako kama akiba kwaajili ya aidha kukuza mtaji wa biashara unayofanya au kuanzisha biashara mpya na malengo mengine ya baadae.


Njia ya pili ni kupitia ndugu wa familia au mrafiki. Wapo wajasiriamali ambao wamefanikiwa kupitia ndugu au marafiki. Kuna msemo unasema hupaswi kumpa mtu samaki bali umfundishe jinsi ya kuvua samaki.

Ndugu wa familia au marafiki ni watu ambao wanaweza kukusaidia kuweza kukuza mtaji kwaajili ya kuanzisha au kuendeleza biashara. Yafaa kutafuta namna bora ya kuweza kukaa na ndugu au rafiki ili kuweza kumshawishi ni kwa namna gani akusaidie.

Ni muhimu kwa mjasiriamali kutoa pendekezo lenye kufaa kwa ndugu au rafiki mwenye uwezo ili kuweza kumshawishi juu ya uwekezaji katika jambo fulani ambalo lina matokeo fulani tarajiwa na vihatarishi vyake na namna ya kuviepuka.

Katika msemo wa usimpe mtu samaki bali mfundishe namna ya kuvua samaki. Maana yake ni kwamba angalia namna unavoweza kumsaidia mtu aweze kujisaidia mwenyewe hasa katika ujasiriamali, si lazima umpatie fedha bali unaweza kumpa vifaa au nyenzo.

Kutumia njia hii ya ndugu au marafiki katika kukuza mtaji wa biashara wakati mwingine kunaweza kuleta matatizo miongoni mwa wana ndugu au marafiki, hivyo katika matumizi ya njia mambo yote yafaa yawekwe wazi ili kuepuka matatizo.

Njia ya tatu ya kuweza kukuza mtaji wa biashara ni kuingia ubia (partnership). Kuingia ubia ni njia inayowakutaniasha watu ambao mahitaji yao yanafana ila upande mmoja unaweza ukawa una hili na mwingine umekosa hili hivyo inabidi kuungana.

Kwa mafano kama wewe una mali X na umekosa mali Y ili kuweza kufanya jambo fulani basi unaweza kuingia ubia na mtu mwenye mali Y ili kila mmoja aweze kufikia malengo yake husika. Makampuni yanaingia ubia itakuwaje kwa nyinyi wajasiriamali!

Pamoja na njia ya ubia kama namna ya kukuza mtaji wa biashara, jambo hili limekuwa gumu kwa watu wengi kwani badala ya kutumia njia hii kujijengea maendeleo wabia wengi wamejikuta wameingia kwenye ‘bifu’ zisizo na msingi na hatimaye kushindwa.

Njia ya nne ya kuweza kukuza mtaji wa biashara ni kutumia mikopo. Hii ni njia kubwa zaidi inayotumiwa na wajasiriamali katika kukuza mitaji ya biashara zao. Ni njia ambayo inahusisha gharama na ambayo imewaacha baadhi ya wajasiriamali katika matatizo.

Wajasiriamali wengi wamekuwa wakitumia Benki, SACCOS, VICOBA na taasisi nyingine za mikopo midogo (Microfinance Institutions) kutafuta fedha ili kuweza kukuza mitaji ya biashara zao. Nashauri, mikopo si ya kukimbilia yafaa kujiuliza kwanza.

Kuepuka matatizo ya kukuza mtaji kwa njia ya mikopo toka taasisi mbalimbali za fedha, yafaa mjasiriamali kujiuliza baadhi ya maswali, lengo kuu la kujiuliza maswali haya ni kuweza kujifanyia tathmini kama kweli unahitaji kukuza mtaji kwa njia ya mkopo.

Swali la kwanza jiulize, je una malengo gani na fedha utakazokopa? Je malengo uliyonayo juu ya mkopo unaoomba yana vihatarishi vipi, hii ni kwasababu taasisi nyingi za fedha hupenda kutoa mikopo kwenye shughuli ambazo zina usalama na endelevu.
Swali la pili la kujiuliza, je unahitaji kiasi gani cha fedha ili kuweza kukuza mtaji wa biashara yako ? Kuna wajasiriamali ambao huenda kukopa lakini hawajui wanahitaji kiasi gani, hawajajipanga ! Wanachojua wanataka kukopa tu, mambo mengine baadae.

Swali la tatu la kujiuliza, ni lini hasa unahitaji mkopo huo ? Wapo ambao wanakopa kwanza halafu baada ya kupata mkopo ndio wanakaa chini kupanga mipango. Kaa chini ujiulize kama kweli unataka mkopo ungependa upate lini huo mkopo na kwanini.

Swali la nne la kujiuliza ni, je utahitaji mkopo huo kwa muda gani ? Kama utahitaji mkopo kwa muda mfupi na kwasababu zinazoeleweka, itakuwa rahisi kwako kushawishi taasisi ya fedha kukupatia mkopo badala ya kukaa bila kujua muda wa hitaji lako.

Swali la tano na la msingi ni juu ulipwaji wa mkopo, ukiomba mkopo na kupewa je utaulipaje ? Je una vyanzo gani vya mapato ambavyo unaweza kuvitumia katika kuhakikisha mkopo unarejeshwa pamoja na gharama zake (riba) kwa muda uliopangwa .

Swali la sita la kujiuliza ni ikiwa mambo yataenda mlama, nini kitafanya mkopo ubaki  salama ? Hapa wakopeshaji wengi huhitaji dhamana za mkopo (collateral) ili kuweza kwa namna moja au nyingine kuulinda mkopo uliotolewa ili ubaki salama, kulipika!

Ni matumaini yangu ndugu mjasiriamali, katika kutafuta namana bora ya kukuza mtaji wa biashara yako utaangalia ile ambayo inaendana na hali halisi uliyonayo badala ya kukurupuka au kufuata mkumbo, kwa njia hii utaweza kuepuka matatizo yasiyo lazima
.
KAMA UNAHITAJI USHAURI WOWOTE KUHUSU BIASHARA UNAWEZA PIGA NAMBA 0658494977


SOURCE: KONA YA MJASIRIAMALI (NIPASHE).

WAKO FARAJA MMASA

+X3p

Share:

0 comments:

Post a Comment

KUHUSU MMILIKI WA BLOG HII

My photo
Naitwa faraja Mmasa a.k.a Moa,Mkazi na mzaliwa wa Wilaya ya Gairo Morogoro.KARIBU KATIKA BLOG hii tuelimishane mambo mbalimbali.Inatupasa kuwa na ufahamu wa mambo mbalimbali ili tuweze kuyatawala Mazingira yetu .Kuwa na Mwanasheria au Mhasibu haimanishi unatikiwa kujua au kufuatilia maswala ya uhasibu na sheria tu.Mfano nyumba yako au ndoa yako hutaindesha kwa taaluma uliyonayo.Vile vile huwezi kuendesha ujasiliamali kwa mafanikio kwa shahada yako ya uhandisi.TUNAANGAMIA KWA KUKOSA MAARIFA

UJUMBE WA LEO

MIUJIZA MINGI INAYOTOKEA KATIKA MAISHA IPO KATIKA MAWAZO,FIKRA,NA IMANI ALIYONAYO MWANADAMU HUSIKA

USIKOSE KIPINDI HOT JIJINI POWER CLUB ,SIBUKA REDIO 94.5 KILA SIKU SAA SABA MPAKA SAA KUMI

USIKOSE KIPINDI HOT JIJINI POWER CLUB ,SIBUKA REDIO 94.5 KILA SIKU SAA SABA MPAKA SAA KUMI

GAR AD2

GAR AD2

GARI ADVERT

GARI ADVERT

Castrol

Castrol
Powered by Blogger.