Saturday, March 28, 2015

Kiri Kosa, Jifunze, Jipe Nafasi Ya Kuanza Upya.


Katika safari ya maisha, ni jambo la kawaida kabisa kukutana na vikwazo vinavyoweza kukatisha tamaa. Ukubwa wa vikwazo au changamoto hizo, zinaweza kukusababishia ukaiona dunia kama imegeuka, au wakati mwingine ukatamani ipasuke uingie ndani yake.
 
Yapo mambo mengi yanayoweza kukufanya ufikirie hivyo. Huenda yakawa ni makosa ya kibinadamu, matatizo, changamoto, kukatishwa tamaa na baadhi ya watu au kujiponza mwenyewe kutokana na hili au lile. Lakini ukikaa chini, ukatafakari utatambua kuwa hakuna binadamu asiyeteleza kwa kufanya makosa au kupitia changamoto kwenye safari ya maisha.

Hivyo wakati mwingine unapaswa kuelewa kuwa kwa kila linalokupata, bado unayo nafasi ya kufungua ukurasa mpya. Kupatwa na mitihani katika maisha, mara nyingi ni darasa mojawapo tunalotakiwa kuliangalia kwa umakini ili kupata somo au fundisho lililo ndani yake.

Ikiwa mtihani huo umekuja kutokana na kosa ulilofanya, ni vyema kukubali kama umekosea na kisha kujipa nafasi ya kusonga mbele. Tunaelewa kuwa maisha ya kila mmoja wetu kwa namna moja au nyingine yanaendeshwa na misimamo mbalimbali. Kuna wale wanaoamini kuwa wao hawawezi kufanya  jambo Fulani na wakati mwingine kuamini kuwa hawawezi kukosea kabisa.


Ni sawa lakini tukumbuke kwamba hakuna binadamu aliyekamilika kwa kila mmoja wetu anaweza kuteleza na kufanya kosa bila kukusudia . Hivyo basi kwa namna yoyote ile katika maisha yetu kutenda makosa ni sehemu ya maisha. Ni vyema kujifunza kukubali kama umekosea na kujirekebisha.

   Pili, jifunze kutokana na lile kosa. Si dhani kama leo ukikosea jambo Fulani unaweza kulirudia kosa kama lile siku nyingine. Hata kama ikitokea labda kwa namna nyingine tena. Nakumbuka wakati nikiwa mdogo baba yangu aliniletea zawadi kama pongezi ya kufanya vizuri darasani.

 Siku hiyo aliponiletea tulikuwa tumekaa na kaka zangu. Alinikaribisha tukiwa pamoja ili iwe chachu kwa wao kufanya vizuri pia. Au pengine kuwafanya waone wivu na wao waweze kufanya vizuri wakiwa shuleni. Basi alinipa ile zawadi. Wakati wa kupokea nilifanya kosa kwa kupokea na mkono wa kushoto. Kwa ukali aliniambia nirudishe ile zawadi akaondoka nayo.

Baada ya kutafakari kwa muda nikakumbuka kumbuka kuwa nilifanya kosa kupokea na mkono wa kushoto kitendo ambacho alishawahi kutusisitizia kuwa siyo cha heshima. Lile lilikuwa funzo kwangu kwani mpaka leo sikuwahi kufahamu ile zawadi ilikuwa ni ya aina gani, kwani ilikuwa imefungwa.

Baada ya kutokea kwa kadhia ile na kuweza kugundua kosa langu, moja kwa moja nilienda kuomba msamaha kwa baba. Tangu siku ile sikuwahi tena kumpa au kupokea kitu chochote na mkono wa kushoto. Hata ikitokea hivyo kama nimejisahau lazima nitaomba radhi.

Ninachoamini mimi ni kwamba kwa hali yoyote ile ni lazima tuyape nafasi maisha yaendelee. Hivyo hatuna haja ya kuangalia nyuma pale tunapojikwaa, kwani utakachoambulia hapo ni maumivu tena inawezekana ukaumia hapo kuliko awali.
Wapo waliofikia kufanya maamuzi ya ajabu baada ya kukutwa na mtihani au kufanya makosa katika jamii. Wengine hata waliweza kutengwa kutokana na makosa yao. Lakini kushindwa kwao kukubali makosa waliyotenda, kulizaa matatizo mengine. Kwani utakuta ili kuondoa aibu iliyo mbele yao, waliamua kukimbia miji yao na hivyo kwenda kuanza maisha sehemu nyingine.

Suluhisho pekee la jambo kama hili ni kuomba msamaha na kujipanga upya. Usikubali kukata tamaa kwa kuanguka mara moja, hata ukianguka mara tatu bado unayo nafasi ya kusimama na kuanza upya na kufanya vizuri hata pengine kuliko mwanzo. Kitu kikubwa jiamini kisha chukua jukumu la kusonga mbele kwa kujiamini zaidi, utabadili maisha yako na utafanikiwa.

  

Makala hii imeandikwa na Suzan Mwillo wa Gazeti la Mwananchi.

Mawasiliano suzanmwillo@gmail.com
Share:

0 comments:

Post a Comment

KUHUSU MMILIKI WA BLOG HII

My photo
Naitwa faraja Mmasa a.k.a Moa,Mkazi na mzaliwa wa Wilaya ya Gairo Morogoro.KARIBU KATIKA BLOG hii tuelimishane mambo mbalimbali.Inatupasa kuwa na ufahamu wa mambo mbalimbali ili tuweze kuyatawala Mazingira yetu .Kuwa na Mwanasheria au Mhasibu haimanishi unatikiwa kujua au kufuatilia maswala ya uhasibu na sheria tu.Mfano nyumba yako au ndoa yako hutaindesha kwa taaluma uliyonayo.Vile vile huwezi kuendesha ujasiliamali kwa mafanikio kwa shahada yako ya uhandisi.TUNAANGAMIA KWA KUKOSA MAARIFA

UJUMBE WA LEO

MIUJIZA MINGI INAYOTOKEA KATIKA MAISHA IPO KATIKA MAWAZO,FIKRA,NA IMANI ALIYONAYO MWANADAMU HUSIKA

USIKOSE KIPINDI HOT JIJINI POWER CLUB ,SIBUKA REDIO 94.5 KILA SIKU SAA SABA MPAKA SAA KUMI

USIKOSE KIPINDI HOT JIJINI POWER CLUB ,SIBUKA REDIO 94.5 KILA SIKU SAA SABA MPAKA SAA KUMI

GAR AD2

GAR AD2

GARI ADVERT

GARI ADVERT

Castrol

Castrol
Powered by Blogger.